IQNA

Waislamu India wabaguliwa zaidi katika kipindi cha janga la corona

22:56 - April 21, 2020
Habari ID: 3472690
TEHRAN (IQNA)- Ubaguzi wa Waislamu nchini India ambao umeongezeka katika miezi ya hivi karibuni sasa umekithiri zaidi wakati huu wa janga la corona.

Katika tukio la hivi karibuni kabisa, kitendo cha hospitali za India cha kukataa kuwapokea akina mama Waislamu ili kuwatibu, kimepelekea mmoja wa watoto wao wachanga kupoteza maisha.

Rizwana Khatun, mwanamke wa Kiislamu amepoteza mtoto wake baada ya kukataliwa kupokelewa na uongozi wa hospitali ya MGM ya jimbo la Jharkhand kwa kisingizio cha kupambana ugonjwa wa COVID-19 au Corona. Kufuatia kitendo hicho, kichanga cha mwanamke huyo kimefariki dunia kutokana na vipigo na majeraha yaliyosababishwa na walinzi wa hospitali hiyo. Hii ni katika hali ambayo mwezi uliopita pia, mtoto mchanga mwingine wa Kiislamu alifariki dunia baada ya hospitali ya serikali ya eneo la Bharatpur, kusini mwa jimbo la Rajasthan kukataa kumpokea mama yake kwa ajili ya kujifungua.

Katika siku za hivi karibuni Wahindu wenye misimamo ya kuchupa mipaka wamekuwa wakitumia vibaya mgogoro wa virusi vya Corona sambamba na kuwatuhumu Waislamu kuwa eti wanapanga njama dhidi ya nchi hiyo, na hivyo kutekeleza wimbi la mashambulidi dhidi yao. Mwezi Februari mwaka huu mji wa New Delhi, ulishuhudia mashambulizi makali ya Wahindu wenye misimamo mikali na kupelekea Waislamu 54 kuuawa.

Mapema mwezi huu pia Wakuu wa serikali ya India walidai kuwa kesi nyingi za COVID-19  nchini humo zimetokana  mjumuiko wa kila mwaka wa Waislamu (Ijtimai)  ambao ulifanyika New Delhi mapema mwezi Machi.

Kufuatia ubaguzi huo Maulana Badruddin, mbunge katika bunge la India amesema kuwa, serikali ya nchi hiyo inatumia vibaya virusi vya Corona kama wenzo wa kuwakandamiza Waislamu.

Badruddin Ajmal amekosoa siasa za serikali ya India za kuwalenga Waislamu wa nchi hiyo, amesema kuwa, hatua ya kuwatuhumu Waislamu kuwa ndio walioeneza virusi vya Corona ndani ya nchi hiyo, haina ushahidi wowote na pia kwamba ni kinyume na maadili. 

3892785

captcha