Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ametuma ujumbe tofauti kwa viongozi wa nchi za Kiislamu akiwapongeza kwa maadhimisho ya Sikukuu ya Idul- Adh'ha. Amesema kuwa, viongozi wa nchi za Kiislamu wanaweza kuleta umoja na mshikamano mkubwa katika Ulimwengu wa Kiislamu chini ya kivuli cha irada na jitihada za pamoja.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa anataraji kwamba Waislamu wote duniani kwa baraka za sikukuu hii adhimu na kwa kufuata mafundisho halisi ya dini Tukufu ya Kiislamu wataweza kuchukua hatua za kumkurubia Mwenyezi Mungu.
Leo tarehe 10 Dhilhaj ni sikukuu ya Idul Adh'ha, moja ya sikukuu kubwa za Kiislamu. Katika siku hii mahujaji wa Nyumba Tukufu ya Mwenyezi Mungu waliokwenda Makka, huchinja mnyama kwa ajili ya kutekeleza amri ya Mola wao na kuhuisha kumbukumbu ya Nabii Mtukufu Ibrahim AS.