IQNA

Mfalme wa Morocco asisitiza kuunga mkono Palestina

21:06 - December 01, 2020
Habari ID: 3473411
TEHRAN (IQNA) - Mfalme Mohammad VI wa Morocco amesema nchi yake itaendelea kuunga mkono Wapalestina hadi watakaporejeshewa haki zao zote hasa kuanzishwa nchi huru ya Palestina mji wake mkuu ukiwa ni Quds (Jerusalem) Mashariki.

“Tunasimama pamoja na watu wa Palestina na tunaunga mkono haki zao za kisheria za kuunda nchi huru ya Palestina mji wake mkuu ukiwa ni Quds Mashariki,” amesema mfalme Muhammad katika ujumbe wake kwa mwenyekiti wa Kamati ya Haki za Watu wa Palestina,  Cheikh Niang.

Ametoa kauli hiyo kwa mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya Kufungamana na Watu wa Palestina, ambayo huadhimishwa Novemba 29 kila mwaka.

Mfalme huyo amesema kadhia ya Palestina ni kadhia muhimu zaidi Mashariki ya Kati na ni kati ya vipaumbele muhimuvya Morocco.

Aidha ameulaani utawala wa Kizayuni wa Israel kwa kuendeleza sera za kupora zaidi ardhi za Palestina kupitia ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni.

Watu wa Morocco walijumuika Jumatatu katika jengo la bunge mjini Rabat Jummatatu kulaani jinai za utawala wa Israel dhidi ya Wapalestina.

Aidha waliteketeza moto bendera za Israel sambamba na kulaani nchi za Kiarabu ambazo zimeanzisha uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni wa Israel.

347328

captcha