IQNA

Maulamaa Waislamu watoa wito wa kuadhimishwa ‘Wiki ya Quds’

20:35 - March 03, 2021
Habari ID: 3473699
TEHRAN (IQNA) – Jumuiya ya Kimataifa ya Maulamaa wa Kiislamu (IUMS) imetoa wito wa kuadhimishwa ‘Wiki ya Kimataifa ya Quds (Jerusalem)’ kwa lengo la kuunga mkono harakati za ukombozi wa Palestina.

Katika taarifa, IUMS imesema wiki hiyo itakayoadhimishwa kote duniani kuanzia Machi 6-12 inaadhimishwa kwa lengo la kuunga mkono harakati za kuukomboa mji wa Quds unaokaliwa kwa mabavu na utawala haramu wa Israel. Katika mji wa Quds ndio uliko msikiti wa Al Aqsa ambao ulikuwa qibla cha kwanza cha Waislamu. IUMS imetoa wito kwa wanazuoni wa Kiislamu, taasisi na vyombo vya habari vya Kiislamu kuadhimisha wiki hii kwa kuelimisha jamii kupitia mihadhara, warsha na vipindi vya televisheni.

Aidha wametoa wito wa kuwepo ushirikiano baina ya wasomi Waislamu na Wapalestina katika kukabiliana na njama za Israel za kuuyahudisha Msikiti wa Al Aqsa na mji wa Quds.

Asasi moja ya kijamii nchini Uingereza inayojulikana kama ‘Marafiki wa Al Aqsa’ imetangaza kuandaa  ‘Wiki ya Quds’ ili kuelimisha jamii kuhusu kadhia ya Palestina.

Utawala wa Kizayuni unatekeleza misingi mitatu mikuu ambayo ni kuugawa utumiaji wa Msikiti wa Al Aqsa kisehemu na kiwakati, kuchimba mashimo ya chini kwa chini na kandokando ya msikiti na kuyahudisha maeneo ya jirani na mahala hapo patakatifu.

Hii ni katika hali ambayo, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) limethibitisha tena kwamba msikiti mtukufu wa Al-Aqsa, kibla cha kwanza cha Waislamu ni milki ya Wapalestina.

3474152

captcha