Katika salamu hizo za pole, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema amesikitishwa mno na habari ya kuaga dunia Jenerali Hijazi, ambapo amemuombea amani na baraka za Allah.
Kiongozi Muadhamu amemuomba Mwenyezi Mungu ampe faraja mjane, watoto, familia na wafanyakazi wenza za Shahidi Hijazi, katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.
Amesema miongoni mwa sifa na tabia alizojipamba nazo Jenerali Hijazi ni moyo wa kujitolea na kupambana, fikra pevu, moyo uliojaa imani ya kweli na ilhamu. Ayatullah Ali Khamenei amesema Brigedia Jenerali Hijazi alisabilia maisha yake katika kuuhudumia Uislamu na Mapinduzi ya Kiislamu.
Mwishoni mwa ujumbe huo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amemuomba Allah amrahamu na kumsamehe madhambi yake Jenerali Hijazi.
Jenerali Hijazi
Naibu Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (IRGC) aliaga dunia Jumapili usiku.
Msemaji wa IRGC, Ramezan Sharif amesema Brigedia Jenerali Mohammad Hosseinzadeh Hijazi, Naibu Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ameaga dunia usiku wa kuamkia leo akiwa na umri wa miaka 65, kutokana na mshtuko wa moyo.
Shahidi Brigedia Jenerali Mohammad Hosseinzadeh Hijazi
Ameongeza kuwa, Shahidi Hijazi ameaga dunia kutokana na athari za kemikali zilizomuingia mwilini wakati wa Vita vya Kujihamu Kutakatifu vilivyoanzishwa na Iraq dhidi ya Iran katika miaka 80.
Msemaji wa IRGC amebainisha kuwa, Brigedia Jenerali Hijazi alikumbwa na ugonjwa wa Covid-19 miezi kadhaa iliyopita. Shahidi Hijazi alikuwa mmoja wa maveterani waliopigana mstari wa mbele katika vita vya kichokozi vilivyoanzishwa na aliyekuwa dikteta wa Iraq, Saddam Hussein kuanzia mwaka 1980 hadi 1988.