Akizungumza Jumatatu mjini Tehran, Nusratullah Lotfi, naibu mkuu wa Baraza la Uratibu wa Ustawi wa Kiislamu amesema kinyume na miaka iliyopita, mwaka huu hakutakuwa na mijumuiko ya Siku ya Kimataifa ya Quds.
Amesema uamuzi huo umechukuliwa kutokana na hali iliyoko hivi sasa ya janga la COVID-19.
Aidha amesema Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyid Ali Khamenei atatoa hotuba maalumu kwa mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya Quds Ijumaa saa tano asubuhi kwa saa za Tehran. Hotuba hiyo itarushwa mubashara na televisheni za kimataifa za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kama vile Al Alam, Press TV, Al Kauthar na Iran Press.
Katika maeneo mengine duniani pia mijimuiko ya Siku ya Kimataifa ya Quds inatazamiwa kufanyika kupitia intaneti kupitia kampeni ya kimatiafa ya kupeperusha bendera ya Palestina iliyopewa hashtegi ya #FlyTheFlag for Palestine
Imam Khomeini MA Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alitangaza kuwa Ijumaa ya mwisho ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni Siku ya Kimataifa ya Quds.
Waislamu na wapenda haki wamekuwa wakifanya maandamano katika pembe mbalimbali za dunia kila mwaka katika Siku ya Kimataifa ya Quds, na kubainisha hasira zao kwa siasa za kibaguzi na kikatili zinazotekelezwa na utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi madhulumu wa Palestina.
Mwaka huu Siku ya Kimataifa ya Quds itakuwa Ijumaa Mei 7.