Kwa mujibu wa taarifa satalaiti hiyo imerushwa katika anga za mbali katika umbali wa zaidi ya kilomita 500 kutoka ardhini.
Hii ni satalaiti ya pili ya kijeshi kurushwa na jeshi la IRGC. Huko nyuma yaani mwaka 2020 Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (IRGC) limewahi kurusha satalaiti ya Nour-1 iliyokuwa satalaiti ya kwanza ya kijeshi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, ambayo ilirushwa umbali wa kilomita 425 kutoka ardhini.
Baada ya leo kurushwa kwa mafanikio satalaiti ya Nour-2, sasa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ina satalaiti mbili za kijeshi katikka anga za mbali ambapo moja iko umbali wa kilomita 425 na nyingine umbali wa kilomita 500 kutoka ardhini.
Iran ilirusha katika anga za mbali satalaiti yake ya kwanza kabisa inayojulikana kwa jina la Omid (yaani Tumaini) mwaka 2009.
Iran pia imetangaza kuwa, katika kipindi cha miaka michache ijayo itatuma mwanaadamu katika anga za mbali. Tayari mazoezi yameshafanyika kuhusiana na lengo hilo kwa kutumwa nyani hai katika anga za mbali ambaye alirejea ardhini akiwa salama.
Mafanikio haya ya Iran katika sekta ya anga za mbali yamepatikana licha ya kuwepo vikwazo vya kila upande vya nchi za Magharibi dhidi ya Jamhuri ya Kislamu ya Iran.