IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Adui ana mpango wa kudhoofisha imani na matumaini

18:13 - June 21, 2022
Habari ID: 3475407
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, mpango wa adui ni kudhoofisha imani na matumaini na kutaka ionekane kwamba viongozi wamefika kwenye mkwamo na hawajui namna ya kuendesha nchi.

Mnamo tarehe 12 Juni, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei aliwahutubia waandalizi wa kongamano la kitaifa la mashahidi wa jamii za jadi za Iran; na hotuba yake hiyo imetolewa na kusomwa leo katika ukumbi wa kongamano hilo linalofanyika katika mji wa Kurdistan mkoani Chahar Mahal na Bakhtiari.

Katika hotuba yake kwa maafisa hao, Ayatullah Khamenei aliashiria kauli ya Imam Khomeini aliyezitaja jamii za jadi za Iran kuwa ni hazina za akiba ya nchi na akasema, kufanyika kongamano hilo ni fursa mwafaka ya kuwafahamisha na kuwaelimisha wananchi kuhusu jami za jadi. 

Alifafanua kwa kusema: leo hii wanaoitakia mabaya Iran na Uislamu wamejikita zaidi katika vita laini (visivyo vya kijeshi), kwa hivyo kuna haja kwa wananchi wote wakiwemo wa jamii za jadi kujishughulisha na masuala ya kiutamaduni na uzalishaji wa kiutamaduni.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria pia kusimama imara jamii za jadi mbele ya njama zisizohesabika za maajinabia katika muda wote wa karne tatu zilizopita na akasema, lengo la njama hizo lilikuwa ni kuwashawishi watu wa jamii za jadi waisaliti nchi na kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kutaka kujitenga na kuanzisha vita vya ndani, lakini hawakufanikiwa katu; kwa hivyo jamii za jadi za Iran ni miongoni mwa matabaka aminifu zaidi ya wananchi.

Ayatullah Khamenei ameeleza pia kwamba, moyo wa kujitolea wa jamii za jadi wakati wa Mapinduzi na katika vita vya Kujihami Kutakatifu ni dhihirisho jengine la kujitoa mhanga jamii hizo na akaongezea kwa kusema: dini, ndio sababu kuu na muhimu zaidi ya kupatikana umoja, maendeleo na moyo wa kujitolea wa wananchi wakiwemo wa jamii za jadi na ndio aliyoitumia Imam Khomeini kuyafikisha Mapinduzi kwenye ushindi; na baada ya Mapinduzi, ndiyo iliyoikinga na kuilinda nchi na msukumo na uungaji mkono wa madola ya kigeni na tawala zenye fikra mgando kwa Saddam, uliokuwa na lengo la kuyasambaratisha Mapinduzi.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekumbusha kuwa kudhoofisha imani ya dini na kudhoofisha matumaini juu ya mustakabali wa nchi ni miongoni mwa mbinu za vita laini vinavyoendeshwa dhidi ya taifa la Iran na akasema: kujaribu kuonyesha kuwa hakuna mustakabali, kuna hali ya mkwamo na kwamba viongozi hawana ujuzi wa kuendesha nchi ni miongoni mwa mambo yanayofanywa na wanaoitakia mabaya Iran.

4065626/

captcha