IQNA

Ibada ya Hija

Maafisa wa Hija wa Iran na Russia wakutana Makka kujadili ushirikiano

17:47 - July 05, 2022
Habari ID: 3475464
TEHRAN (IQNA) – Wasimamizi wa Hija nchini Iran wamekutana na wenzao wa Russia mjini Makka na kufanya mazungumzo kuhusu njia za kuongeza ushirikiano wa pande mbili.

Naibu mkuu wa Ujumbe wa Hija wa Russia Mousa Asiyov ametembelea Ofisi ya Mwakilishi wa Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu mjini Mecca, na kufanya mazungumzo na naibu mkuu wa ofisi hiyo Hujjatul Islam Seyyed Hussein Roknedini.

Afisa huyo wa Russia alisema kwamba ofisi yake na familia za Mahujaji hutumia apu maalumu ya simu za mkononi kupata taarifa kuhusu hali za Mahujaji wa Russia.

Amebainisha masikitikio yake kuwa ibada ya Hija ilisita kwa muda wa miaka miwili kutokana na janga la COVID-19. Asiyov pia aliwasilisha ripoti fupi kuhusu hali ya Waislamu wa Russia katika Hija ya mwaka huu na pia baadhi ya shida ambazo walikumbana nazo wakati wa kuwatuma Mahujaji.

Kwa upande wake, Hujjatul Islam Roknedini aliitaja Hija kuwa fursa ya kukutana na Waislamu, akibainisha kuwa mikutano na mashauriano yanaweza kuandaa mazingira ya kupanuka kwa uhusiano kati ya mataifa na serikali.

Afisa huyo wa Iran alitaja kupunguzwa kwa idadi ya Mahujaji pamoja na kuongezwa gharama kuwa changamoto kubwa ambazo "zimewatia wasiwasi" Waislamu mwaka huu.

Akirejelea uzoefu wa ujumbe wa Iran katika Hija katika kutoa huduma kwa Mahujaji katika nyanja za mafunzo, upishi, na masuala ya matibabu, Hujjatul Islam Roknedini alialika wajumbe wa Russia kutembelea vituo vya matibabu vya Iran na kituo cha huduma za chakula kwa Mahujaji mjini Makka.

Alielezea utayari wa Iran kubadilishana uzoefu wake na Russia kupitia warsha za mafunzo.

Zaidi ya hayo, aiashiria pia uwepo wa Msafara wa Qur'ani wa Iran wa Nur huko Makka, akibainisha kwamba kundi hilo linaweza kuandaa programu za Qur'ani kwa ajili ya Mahujaji wa Russia pia.

4068587

captcha