IQNA

Shakhsia katika Qur'ani/3

Hadhrat Adam (AS): Asiyetenda dhambi au Mtenda dhambi?

13:28 - September 26, 2022
Habari ID: 3475841
TEHRAN (IQNA) - Kwa mujibu wa mafundisho ya Uislamu, hakuna Mtume wa Mwenyezi Mungu aliyefanya dhambi au kosa lolote. Ikiwa ndivyo, mtu anawezaje kueleza na kuhalalisha uasi wa Nabii Adam (AS)?

Baada ya kuumbwa kwa Adamu na Hawa, Mwenyezi Mungu aliwaweka katika janna  au paradiso, akiwaambia wale na kufaidika na kila baraka huko lakini wasiukaribie mti uliokatazwa.

Hata hivyo, Shetani aliwadanganya na wakala matunda ya mti uliokatazwa. Kwa sababu ya kutotii kwao, walifukuzwa kutoka paradiso na kuishi duniani.

Quran Tukufu inaelezea hatua ya Adam (AS) kuwa ni uasi: "... Na Adam akamuasi Mola wake Mlezi, na akapotea njia." (Sura Taha, aya ya 121)

Adam (AS) alikuwa nabii wa kwanza na, kwa mujibu wa imani ya Waislamu wa madhehebu ya Shia, Manabii wa Mungu kamwe hawatendi dhambi au makosa. Kwa hiyo ni vipi tueleze kutotii kwa Adam? Kuna maoni matano kuhusu nukta hii  katika tafsiri za Qur'ani za Kishia:

1- Makosa yaliyofanywa na Mitume kama Adam (AS), Yusuf (AS), Yunus (AS), ..., sio dhambi bali ni Tark al-Awla (kuacha bora). Uasi haimaanishi kufanya dhambi kwa kuacha Wajib (wajibu) au kufanya jambo la Haram (iliyoharamishwa), bali inaweza kumaanisha kuacha jambo ambalo ni Mustahab (lililopendekezwa) au kufanya jambo ambalo ni Makruh (bora kuliepuka). Kwa hiyo uasi wa Adam ulikuwa ni kitendo cha Makruh lakini kwa sababu Mitume wana hadhi tukufu, hata kufanya kitendo cha Makruh haitarajiwi kutoka kwao na wakifanya hivyo, Mwenyezi Mungu anawakemea.

2- Wengine wanaamini kuwa Mwenyezi Mungu aliwaamuru Adamu na Hawa wasile matunda ya mti huo ili watambue matokeo ya asili ya kitendo hicho. Mgonjwa asipofanya kulingana na kile anachoambiwa na daktari, hatakuwa na adhabu bali atapata madhara.

Quran inasema: "  Tukasema: Ewe Adam! Hakika huyu ni adui yako na wa mkeo. Basi asikutoeni katika Bustani hii, mkaingia mashakani.” (Sura Taha, aya ya 117)

3- Baadhi ya wafasiri wa Qur’ani wanasema kuwa kumkataza Adam asiukaribie mti na kula matunda yake haikuwa amri bali ni pendekezo tu. Ndio kusema, wanaamini kuwa kilikuwa ni kitendo cha Mustahab kukwepa kula tunda hilo, na Adam (AS) alijinyima Thawab (malipo) yake kwa alichokifanya.

4- Baadhi ya wengine wanasema kuwa kisa cha Adam (AS) na uasi wake ni mfano unaoashiria ubinadamu sio Adam (AS) mwenyewe.

5- Baadhi ya wafasiri wengine wa Qur'ani wanarejea kwenye Hadith na kusema uasi wa Adam (AS) ulifanyika kabla ya Bi'tha (kuteuliwa kwake kuwa Mtume).

captcha