Duru za usalama za utawala huo sambamba na kukiri juu ya wasi wasi mkubwa lililonao jeshi la utawala huo wa kuingia vitani wakati mmoja na harakati hizo zimetangaza kwamba, bila shaka Tel Aviv inakabiliwa na ukweli ulio wazi kwamba 'vita vijavyo vitakuwa tofauti kabisa.' Aidha duru za usalama ndani ya utawala wa Kizayuni pia zimeashiria juu ya uwezo mkubwa wa harakati za Hamas na Hizbullah wa kumiliki ndege zisizo na rubani na kusema kuwa, kwa kuwa na makombora yanayolenga shabaha kwa umakini mkubwa, harakati ya Hizbullah inaweza kuvishambulia vituo vya kibiashara na majengo ya Wizara ya Vita ya Israel ndani ya Tel Aviv, ambao ni mji mkuu wa utawala huo bandia.
Kabla ya hapo pia naibu wa zamani wa mkuu wa Shirika la Kijasusi la Utawala wa Kizayuni wa Israel (MOSSAD) ambaye pia ni mbunge katika bunge la utawala huo (Knesset) alikiri udhaifu na kushindwa Israel mbele ya harakati ya muqawama ya Hamas ya Ukanda wa Gaza.