Akitoa radiamali yake kuhusiana na wito wa Wazayuni wa kuvamia msikiti wa al-Aqswa, Mufti Mkuu wa Quds ameonya kuwa, Wazayuni wanafanya njama za kubadilisha utambulisho wa msikiti huo mtakatifu na kuwatwisha walimwengu kitu kingine ambacho kinakwenda kinyume na uhalisia wa mambo.
Sheikh Mohamed Ahmed Hossein Mufti Mkuu wa mji wa Quds huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu amesisitiza kuwa, makundi ya Wazayuni yanafanya njama za kubadilisha ukweli wa mambo jambo ambalo halikubaliki hata kidogo. Hayo yanajiri sambamba na kushadidi hujuma na uvamizi wa walowezi wa Kizayuni katika msikiti huo.
Kwa mujibu wa duru za Kipalestina, karibu kila siku walowezi wa Kizayuni wamekuwa wakifanya uvamizi katika msikiti huo lengo likiwa ni kutekeleza njama za kutokomeza utambulisho wa Kiislamu na Kikristo wa Msikiti wa al-Aqswa na badala yake kuweka nembo za Kizayuni.
Katika miaka ya hivi karibuni, utawala wa Kizayuni wa Israel umeshadidisha hujuma na uvamizi wake dhidi ya maeneo ya Wapalestina, ukifanya njama za kufikia malengo yake haramu katika ardhi za Wapalestina.
Hata hivyo kusimama kidete wananchi wa Palestina hadi sasa kumekwamisha njama na mipango yote ya Wazayuni, zikiwemo njama zake za kubadilisha muundo wa kijamii na kijiografia wa Baytul Muqaddas.