IQNA

Rais wa Afghanistan akanusha mpango wa kuwaachia huru wafungwa 5,000 wa Taliban

12:03 - March 01, 2020
Habari ID: 3472518
TEHRAN (IQNA) – Serikali ya Afghanistan imesema haina mpango wa kuwaachia huru wafungwa 5,000 wa kundi la Taliban pamoja na kuwa nukta hiyo imetajwa katika mapatano ya Marekani na wanamgambo wa Taliban.

Akizungumza Jumapili, Rais Ashraf Ghani wa Afghanistan amekanusha kuwepo mpango kama huo na kusisitiza kuwa takwa la Taliban la kutaka wafungwa hao waachiliwe huru kabla ya mazungumzo ya ana kwa ana haliwezi kutekelezeka kwa sasa.

Duru za habari nchini Afghanistan zimearifu kwamba serikali ya Kabul na kundi la Taleban zimekubaliana kuanza mazungumzo ya amani baina yao.Kwa mujibu wa habari hiyo, mazungumzo hayo ya amani yataanza rasmi tarehe 10 Machi mwaka huu. Hayo yamesemwa na Mullah Abdul Ghani Beradar, Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa wa Kundi la Taleban nchini Qatar na kuongeza kuwa, kundi hilo linaziita pande zote kwa ajili ya mazungumzo hayo. Hayo yanajiri ambapo leo wawakilishi wa kundi la Taleban na Marekani wametiliana saini ya kuhitimisha vita na mapigano nchini Afghanistan huko mjini Doha, Qatar ambayo kwa mujibu wake imepangwa kuwa wapiganaji wa Taleban watatakiwa kupunguza mapigano yao na mkabala wake kuhakikisha askari wa Marekani na wa kigeni wakiondoka kikamilifu ndani ya miezi 14 ijayo kutoka nchi hiyo.

Soheil Shahen, Msemaji wa Ofisi ya Kisiasa ya Taleban sambamba na kusisitiza kwamba kundi hilo litatekeleza ahadi zake zote kwa mujibu wa makubaliano yaliyotiwa saini, amesema kuwa katika mazungumzo yenye lengo la kufikiwa amani na kuainisha muundo wa kisiasa nchini Afghanistan, pande zote za kisiasa nchini humo zitashirikishwa. Kufuatia utiaji saini huo Hamid Karzai, Rais wa Zamani wa Afghanistan amesema, mwenendo wa amani unatakiwa kusimamiwa na kutekelezwa na raia wenyewe wa nchi hiyo. Makubaliano hayo yametiwa saini katika hali ambayo hadi sasa hatua za Marekani nchini Afghanistani si tu kwamba hazijawahi kuwa na faida yoyote kwa raia wa nchi hiyo, bali hatua zake za kijinai na mauaji ya kutisha, vimeitumbukiza nchi hiyo ya Asia katika ghasia, vita na machafuko makubwa.

3470791

captcha