IQNA

Fatwa ya Ayatullah Khamenei kuhusu Saumu ya Ramadhani wakati wa janga la corona

13:02 - April 19, 2020
Habari ID: 3472682
TEHRAN (IQNA) – Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyed Ali Khamenei amejibu swali (Istifta) kuhusu Saumu ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani katika mazingira ya sasa ya kuenea janga la COVID-19 au corona duniani.

Kwa mujibu wa tovuti ya Kiongozi Muadhamu, Istifta ilihusu kufunga Saumu ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa kuzingatia kuenea janga la COVID-19.

Katika kujibu, Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa Saumu ya Ramadhani ni wajibu kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwa hakika pia ni neema maalumu ya Mwenyezi Mungu kwa waja wake. Halikadhalika amesema sumu ni msingi wa kukamilika roho ya mwanaadamu mbali na kuwa ilikuwa wajibu kwa umma zilizotangulia kabla ya Uislamu.

Aidha Ayatullah Khamanei amesema kati ya taathira chanya za saumu ni kujitokeza umaanawi wa batini, taqwa ya mtu binafsi na jamii na huimarisha irada na moyo wa kimuqawama au kimapambano mbele ya masaibu. Halikadhalika amesema Saumu inaimarisha afya ya mwili wa mwanadamu mbali na kuwa Mwenyezi Mungu SWT amewajaalia ujira mkubwa wenye kufunga.

Ayatullah Khamenei amebainisha kuwa, saumu ni moja kati ya misingi na dharura katika Uislamu na hivyo kuacha kufunga Saumu ya Mwezi wa Ramadhani ni jambo lisilokubalika isipokuwa tu mtu awe na yakini ya kimantiki kuwa saumu itapelekea apate ugonjwa au ugonjwa kushadidi, au kuongezeka muda wa ugonjwa au kuchelewa kupona. Ayatullah Khamenei amesisitiza kuwa katika kuamua kutofunga Saumu ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani inatosha kufuata maagizo ya daktari mtaalamu na mcha Mungu.

Kwa hivyo iwapo mtu ana hofu na hofu hiyo ikawa na msingi wa kimantiki, katika hali kama hiyo inakubalika kutofunga lakini ni lazima kulipa baadaye siku ambazo hakuweza kufunga.

3892505

captcha