Kwa mujibu wa taarifa, wafanyaziara kadhaa wameuawa na wengine kujeruhiwa katika hujuma hiyo iliyojiri katika mkesha wa kukumbuka kuuawa Shahidi Musa ibn Ja'far al-Kadhim AS. Baadhi ya taarifa zinasema mwanamke mmoja ameuawa shahidi katika tukio hilo
Duru za usalama zinadokeza kuwa wafanyaziara hao wa Imam Musa Kadhim AS walishambuliwa kwa gurunedi.
Walioshuhudia wanasema gaidi aliyewavurumishia wafanyaziara gurunedi alikamatwa na maafisa wa usalama.
Hujuma hiyo imejiri katika mtaa unaojulikana kama 'Daraja la al-Aimmah' mkoani Baghadad.
Idara ya Usalama ya Iraq aidha imesema watu watatu walikamatwa mapema jana baada ya kubainika kuwa kulikuwa na mpango wa kutekeleza hujuma za kigaidi dhidi ya wafanyaziara wa Imam Kadhim AS.
Idara ya Usalama Baghadad imesisitiza kuwa wafanyaziara leo wataendelea na msafara wao kuelekea katika Msikiti wa Al Kadhimiya.
Masaa machache baada ya tukio hilo Waziri Mkuu wa Iraq Mustafa al Kadhimi ametemeblea eneo la tukio.
Pamoja na kuwa kundi la kigaidi la ISIS au Daesh limeangamizwa nchini Iraq, lakini bado kuna mabaki ya kundi hilo la kigaidi katika maeneo mbali mbali ya Iraq ambao hutekeleza mashambulizi katika baadhi ya maeneo.