IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Iran imemshinda adui katika medani za kisiasa, kijeshi na kiusalama na itamshinda katika vita vya kiuchumi

11:52 - November 20, 2019
Habari ID: 3472222
TEHRAN (IQNA) – Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amelihutubu taifa la Iran pamoja na marafiki na maadui wa mapinduzi na kusisitiza kuwa, wote, wakiwemo marafiki na maadui wa mapinduzi wafahamu kuwa, kuhusiana na medani ya kijeshi, kisiasa na kiusalama -kama vitendo vya machafuko na uharibifu vilivyotokea hivi karibuni hapa nchini ambavyo havikufanywa na wananchi wa kawaida- tumemuacha nyuma adui na kwa fadhila za Mwenyezi Mungu tutamshinda adui huyu pia katika medani ya vita vya kiuchumi.

Ayatulllah Ali Khamenei amesema hayo usiku wa Jumanne mjini Tehran alipokutana na wazalishaji, wajasiriamali na wanaharakati wa masuala ya kiuchumi ambapo sambamba na kuashiria vita vya daima vya kiuchumi baina ya madola makubwa amesema kuwa, katika kipindi cha sasa cha uongozi wa Rais Donald Trump wa Marekani, vita hivi vimepanuka zaidi dhidi ya China, Korea, Ulaya na maeneo mengine na mkabala na Iran vimekuwa vikiendeshwa kupitia kuliwekkea vikwazo taifa hili.

Ayatullah Khamenei amesema kuwa, kuyazatiti mapinduzi kwa silaha ya irada ya uzalishaji wa ndani ndio ufumbuzi wa matatizo haya na akaongeza kuwa, njia pekee ya kuyapatia ufumbuzi matatizo yaliyopo ni kuendelea kuimarisha njia ya uzalishaji wa bidhaa za ndani kwa nguvu zote na kuchukua maamuzi sahihi sambamba na kuondoa vizingiti katika njia hii ambapo athari chanya za harakati hii zinashuhudiwa ukilinganisha na huko nyuma.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran aidha ameashiria umuhimu wa utajiri wa kitaifa na kuenezwa ustawi kwa wote katika Mfumo wa Kiislamu na udharura wa kutokuwa na matumaini kutoka nje na kusisitiza kwamba, kazi na msingi muhimu wa kuukinga uchumi na madhara ya vikwazo ni kuimarisha uzalishaji wa ndani na kwamba, amesimama kidete kuunga mkono hilo na amekuwa akitetetea maendeleo na ustawi wa kweli wa nchi.

Inafaa kuashiria hapa kuwa, katika siku za hivi karibuni, baadhi ya miji ya Iran imeshuhudia ukosefu wa usalama kufuatia uamuzi wa viongozi wa mihimili mitatu ya dola kutekeleza mpango wa usimamizi bora wa mafuta ya petroli. Matukio hayo chungu ambayo yaliandamana na ghasia na utumiaji mabavu na hivyo kupelekea kuharibiwa au kuteketezwa baadhi ya maeneo ya umma pia yamepelekea watu kadhaa ya kupoteza maisha.

3469919

captcha