IQNA

Bunge la Iran laafiki muswada kukabiliana na jinai za utawala wa Kizayuni

12:50 - May 19, 2020
Habari ID: 3472779
TEHRAN (IQNA) - Majlisi ya Ushauri ya Kiisalmu (Bunge la Iran) imeidhinisha muswada wa namna ambavyo Iran itakabiliana na jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel katika upeo wa kitaifa na kimataifa.

Mnamo Mei 12 Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ilipasisha kwa kauli moja muswada wa dharura wa kukabili njama za utawala wa Kizayuni wa Israel, dhidi ya amani na usalama wa kieneo na kimataifa. Muswada huo ulikabidhiwa Kamati ya Usalama wa Taifa na Sera za Kigeni ili kufanyiwa uchunguzi. Kamati hiyo imeufanyia muswada huo marekebisho na sasa unajulikana  kama "Muswada wa Kukabiliana na Hatua za Utawala wa Kizayuni ambazo Zinavuruga Amani na Usalama."

Muswada huo unazitaka taasisi zote za kitaifa za Iran kutumia uwezo wote wa kitaifa na kimataifa kukabiliana na vitendo vya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya taifa linalodhulumiwa la Palestina na mataifa mengine ya Kiislamu ikiwemo Iran. 

Aidha muswada huo unataka kuchukuliwe hatua za kukabiliana na nafasi ya Israel katika kuvuruga usalama na amani kieneo na kimataifa.

Hali kadhalika Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imetakiwa kutayarisha ufunguzi wa Ubalozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Palestina Katika Intaneti katika kipindi cha miezi sita ijayo.

Katika kikao cha leo bungeni, Wabunge wa Iran wamepitisha kwa kauli moja muswada huo huku nara za  'Mauti kwa Israel' zikirindima bungeni.

Jukumu la utekelezwaji muswada huo limekabidhiwa Baraza la Usalama wa Taifa la Iran.

3899740

captcha