IQNA

Waislamu wanapaswa kufanya juhudi za kuwafunza Qurani wasio Waislamu

16:15 - January 19, 2009
Habari ID: 1733138
Iwapo kila Muislamu atamfunza Qur'ani mtu mmoja asiyekuwa Muislamu kila mwaka na kumpa nakala ya Qur'ani atawafunza karibu watu 60 kitabu hicho cha Mwenyezi Mungu katika kipindi cha maisha yake.
Hayo yamesemwa na Abdulrahiim Muhammad Maulana, mtarjumu wa kwanza wa Qur'ani kwa lugha ya Telugu inayotumiwa kwa wingi huko India. Amesema kuwa iwapo kila Muislamu atafanya kazi hiyo tunaweza kuelimisha dunia maarifa ya Qurani Tukufu.
Muhammad Maulana ameashiria kuwa kitabu cha Injili kimetarjumiwa kwa lugha 150 tofauti na kwamba Qur'ani Tukufu imetarjumiwa kwa lugha 50 hadi 60 tu na kusisitiza kuwa, Waislamu wanaweza kutayarisha mazingira mazuri ya kueneza mafunzo ya kitabu cha Qur'ani kwa kutarjumu kitabu hicho kwa lugha mbalimbali.
Tarjumi ya Qurani kwa lugha ya Telugu iliyochapishwa hivi karibuni huko Jiddah Saudi Arabia imechukua kipindi cha miaka 12 na tayari nakala elfu tano za tarjumi hiyo zimekwishauzwa.
Karibu watu milioni 98 wa India na zaidi ya milioni 5.5 katika meneo mbalimbali duniani wanazungumza lugha ya Telugu na wengi kati yao hawajui lugha nyingine ghairi ya hiyo. 350363

captcha