IQNA

Baadhi ya misikiti Indonesia yakaidi amri kuhusu sala za jamaa

17:13 - May 15, 2020
Habari ID: 3472768
TEHRAN (IQNA) – Baadhi ya misikiti imekaidi amri ya serikali ya nchi hiyo kuzuia kwa muda sala za jamaa katika misikiti ili kukabiliana na ugonjwa ambukizi wa COVID-19 au corona.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Indonesia Tito Karnavian amesema bado sala za jamaa zinafanyika katika baadhi ya misikiti nchini humo na kuongeza kuwa imekuwa vigumu kutekeleza agizo la kufunga misikiti. Amesisitiza kuwa hawajapiga marufuku harakati za kidini bali kile kinachozuiwa ni mijumuiko ya watu wengi ambayo ni hatari kutokana na uwezekano wa kusambaza ugonjwa wa COVID-19.

Huko Surabaya, mji mkuu wa jimbo la Java Mashariki, kumeripotiwa kiwango kikubwa zaidi cha maambukizi ya COVID-19 nchini Indonesoa  nje ya mji mkuu Jakarta. Moja ya sababu imetajwa kuwa ni kuendelea kufunguliwa msikiti maarufu wa mjini hum unaojulikana kama Sunan Ampel.

Wakuu wa Surabya wanasema kati ya misikiti 2504, kuna misikiti 386 ambayo imekaidi amri na ingali inaendeleza sala za Ijumaa na Tarawih.

Katika mji mkuu wa Indonesia, Jakarta, watu zaidi ya 5,000 wameambukizwa COVID-19 na ingawa misikiti mingi imetii amri ya serikali ya kuwataka waumini waswali majumbani, bado kuna baadhi ya misikiti ambayo imekaidi amri hiyo.

Indonesia ni nchi yenye idadi kubwa  zaidi ya Waislamu ambayo wanakadiriwa kuwa takribani asilimia 90 ya watu wote milioni 267  nchini humo.

Kwa ujumla watu 16,496 wameambukizwa corona nchini Indonesia huku 1,076 wakifariki dunia.

3471427

captcha