IQNA

Iran yajiunga na dunia kulaani hujuma ya kigaidi Austria

16:46 - November 03, 2020
Habari ID: 3473326
TEHRAN (IQNA) - Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani shambulizi la kigaidi lililotokea nchini Austria na kusema kuwa, kuna udharura wa kuwepo ushirikiano wa jamii ya kimataifa kwa ajili ya kukabiliana na mizizi ya ugaidi.

Katika taarifa, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran Saeed Khatibzadeh ametuma salamu za rambiambi kwa serikali na familia za wahanga wa shambulizi hilo la kigaidi nchini Austria na kusema kuwa: Ugaidi katika sura zake zote unapaswa kulaaniwa, na tukio la jana usiku mjini Vienna limeonyesha tena kwamba, ugaidi na misimamo ya kufurutu ada havitambui mipaka ya nchi.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ya Iran amesema kuwa Kutumia chuki na uchochezi badala ya mantiki na busara vinatengeneza mazingira yasiyo salama ya kusambaa zaidi misimamo ya kuchupa mipaka na ukatili. 

Saeed Khatibzadeh amesisitiza kuwa, kuna udharura wa kuwepo ushirikiano wa jamii ya kimataifa kwa jili ya kupambana na mizizi ya ugaidi na kuongeza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran daima imekuwa sehemu ya juhudi hizo. 

Watu wanne, akiwemo gaidi mmoja, wameuawa na wengine wasiopungua 15 kujeuhiwa katika shambulizi hilo lililolenga maeneo sita ya Jiji la Vienna. 

Vyombo vya usalama vya Austria vimeripoti kuwa, hujuma hiyo imetekelezwa na watu kadhaa waliokuwa na silaha na kwamba mmoja wa wahalifu hao ameuawa, mwingine mmoja ametiwa nguvuni na wenzao kadhaa wametoweka. Imeripotiwa kuwa mashambulizi hayo sita yamefanyika kwa wakati mmoja.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Austria, Karl Nehammer amesema polisi mmoja amejeruhiwa vibaya katika hujuma hiyo. Nehammer ameongeza kuwa, mashambulizi hayo yamefanywa na watu wenye mfungamano na kundi la kigaidi la Daesh au ISIS. Hali ya majeruhi saba wa hujuma hiyo imeripotiwa kuwa mbaya. 

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres amelaani vikali hujuma hiyo na kutuma salamu za rambirambi kwa familia za wahanga. 

615744

captcha