IQNA

Mswada wa sheria za chapa na usambazaji Qur'ani wawasilishwa katika bunge la Misri

18:21 - May 05, 2012
Habari ID: 2318774
Yassir Swalah al-Qadhi, mbunge wa Misri amewasilisha bungeni humo mswada maalumu wa sheria zinazohusiana na uchapishaji pamoja na usambazaji wa Qur'ani Tukufu pamoja na hadithi za Bwana Mtume (saw).
Kwa mujibu wa tovuti ya almesryoon, al-Qadhi amesema kuwa sheria nambari 102 ya mwaka 1985 haina uwezo wa kuzuia uzembe katika uchapishaji na usambazaji wa Qur'ani Tukufu wala njama za baadhi ya watu wanaotaka kupotosha mafundisho ya kitabu hicho kitakatifu. Kwa msingi huo amesema ameona kwamba kuna haja ya kuwasilisha sheria nyingine bungeni ambayo itazuia tatizo hilo.
Al Qadhi Amesema hatua yake hiyo imechochewa pia na hatua ya baadhi ya mashirika kuchapisha nakala za Qur'ani zilizo na makosa ya chapa. Ameongeza kuwa suala hilo linabainika wazi katika hatua ya Jumuiya ya Utafiti wa Kiislamu ya al-Azhar ya kukusanya karibu nakala 20,000 za Qur'ani zilizokuwa na makosa ya chapa kwenye aya, maneno na kurasa zake.
Bwana al-Qadhi amesema mashirika mengi ya uchapishaji Qur'ani nchini Misri hayana vibali vya kuchapisha kitabu hicho cha mbinguni na kwamba huwa hayajali, kuchunguza wala kudhibiti kwa makini nakala za Qur'ani zinazochapishwa kabla na baada ya uchapishaji wake. Amesema kwa kawaida nchini Misri mashirika mengi huzidisha shughuli zao za kuchapisha Qur'ani katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Kwa mujibu wa mswada huo kifungo cha miaka 15 jela na faini kubwa ya pesa kimeainishiwa watu wanaopotosha kwa makusudi maandishi ya Qur'ani wakati wa uchapishaji. 998789
captcha