IQNA

Balozi wa Marekani nchini Yemen awekewa vikwazo na Iran

22:05 - December 10, 2020
Habari ID: 3473443
TEHRAN (IQNA) - Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetangaza kumuweka balozi wa Marekani nchini Yemen katika orodha ya waliowekewa vikwazo na Iran.

Balozi wa Marekani nchini Yemen awekewa vikwazo na Iran

Katika taarifa Jumatano, Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema: "Christopher Henzel, Balozi wa Marekani nchini Yemen amehusika katika kuongoza vita haribifu, mauji ya watu wasio na hatia na waliodhulumiwa na pia kutoa uungaji mkono wa kifedha, silaha na kisiasa kwa muungano vamizi ambao unahusika katika vita dhidi ya Yemen. Taarifa hiyo pia imesema mwanadiplomasia huyo wa Marekani anahusika katika vikwazo vya kinyama na vilivyo dhidi ya watu wa Yemen huku akichochea mgawanyiko wa Yemen sambamba na kuweka vizingiti katika kufikiwa utatuzi wa kisiasa wa mgogoro wa Yemen. Taarifa hiyo ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema hatua hizo za balozi huyo zimesababisha maafa ya kibinadmau nchini Yemen, maafa ambayo yametajwa kuwa janga kubwa zaidi duniani katika karne hii.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imesema balozi huyo wa Marekani amewekewa vikwazo kwa mujibu wa sheria  ya 'Kukabiliana na Hatua za Kigaidi na Ukiukwaji wa Haki za Binadamu Unaofanywa na Marekani.'

Siku ya Jumanne, Wizara ya Fedha ya Marekani ilitangaza kuwa, Hassan Irloo, Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran nchini Yemen anawekewa vikwazo kwa kisingizio kuwa anaunga mkono shughuli za Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC).

Ikumbukwe kuwa mnamo mwezi Machi 2015 muungano wa nchi kadhaa za Kiarabu ukiongozwa na Saudi Arabia na ukiungwa mkono na  Marekani, uliivamia kijeshi Yemen na kuiwekea mzingiro wa kila upande.

Saudia ilianzisha mashambulizi dhidi ya Yemen kwa lengo la kuiondoa madarakani Harakati ya Ansarullah na kumrejesha madarakani Abdrabbuh Mansour Hadi, rais wa zamani wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kukimbilia Riyadh. Hata hivyo hadi sasa Saudia na washirika wake wameshindwa kufikia malengo yao kutokana na kusimama kidete wananchi wa Yemen.

 Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA) hivi karibuni ilitangaza kuwa vita vya Saudi Arabia dhidi ya Yemen vimepelekea zaidi ya watu 233,000 kupoteza maisha katika kipindi cha miaka sita iliyopita.

Wiki iliyopita pia, wakuu wa Yemen walitoa tahadhari kuhusu hali mbaya ya kibinadamu inayozidi kuwa mbaya nchini humo kutokana na vita vinavyoongozwa na Saudi Arabia dhidi ya nchi hiyo masikini ya Kiarabu ambapo 'mtoto mmoja wa Yemen hupoteza maisha kila dakika 10'. Hiyo ni sehemu tu ya jinai za muungano wa kivita wa Saudia-Marekani dhidi ya watu wa Yemen.

2948616

captcha