IQNA

Hisia mseto baada ya ICC kusema ina haki ya kusikiliza kesi ya Palestina dhidi ya Israel

16:44 - February 06, 2021
Habari ID: 3473626
TEHRAN (IQNA)- Kumekuwa na hisia mseto baada ya Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC kutoa hukumu kwa manufaa ya ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni.

Majaji wa mahakama ya ICC, Ijumaa wamesema kuwa, mahakama hiyo ina haki ya kisheria ya kufuatilia jinai na uhalifu uliofanywa na Wazayuni katika ardhi za Palestina mwaka 1967.

Benjamin Netanyahu, waziri mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel ameshindwa kuficha hasira zake kufuatia hujumu hiyo ya Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC yenye makao yake The Hague, Uholanzi.

Netanyahu amekasirishwa sana na hukumu hiyo ya ICC na kusema kwamba mahakama hiyo imethibitisha kuwa ni kundi la kisiasa na si taasisi ya kimahakama.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina imeipokea vizuri hukumu hiyo na kusema kuwa jana usiku ilikuwa ni siku ya kihistoria ya kuanza kufuatiliwa kisheria wahalifu Wazayuni na kwamba mamlaka hiyo iko tayari kutoa ushirikiano wowote utakaohitajiwa na mahakama hiyo ya kimataifa.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani nayo imeelezea wasiwasi wake kufuatia hukumu hiyo ya Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC ambayo ni dhidi ya Israel.

Wananchi wa Palestina wameihesabu hukumu hiyo kuwa ni ya kihistoria hasa kutokana na madhara na hasara kubwa walizosababishiwa na jinai zisizo na kifani za Wazayuni.

Hukumu ya makama ya ICC imesema, ardhi za Wapalestina zilizotekwa na Wazayuni mwaka 1967 zinajumuisha eneo lote la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan ikiwemo Baytul Muqaddas Mashariki, Ukanda wa Ghaza n.k, na kwamba vitongoji vyote vya walowezi wa Kizayuni vilivyojengwa, vinavyojengwa na vitakavyojengwa kwenye ardhi hizo ni haramu na ni kinyume cha sheria.

3952254

captcha