IQNA

Qur'ani Tukufu inauchukulia uchochezi wa kimakundi kuwa kufri kubwa zaidi

21:06 - October 19, 2010
Habari ID: 2016070
Ayatullah Seyyid Abul Qasim Dibaji, Katibu Mkuu wa Baraza la Kimataifa la Fiqhi ya Kiislamu amesema uchochezi wa kimakundi ni kufri kubwa zaidi kwa mtazamo wa mafundisho ya Qur'ani.
Akizungumzia suala hilo hivi karibuni huko Kuwait, Ayatullah Dibaji alisisitiza juu ya umuhimu wa kubainishwa wazi misingi na matawi ya dini yanayowaunganisha Mashia na Masuni. Akizungumza mbele ya wawakilishi wa vyombo vya habari na idadi kadhaa ya wanazuoni, Ayatullah Dibaji amesema kuwa kuzusha fitina miongoni mwa Waislamu na kuwagawa katika makundi ni kufri kubwa zaidi kwa mtazamo wa Qur'ani Tukufu. Amesema, baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikihubiri fitina na siasa za kuwatenganisha Waislamu kwa kusisitiza juu ya hitilafu ndogondogo zilizopo kati ya Waislamu.
Ayatullah Dibaji ambaye pia ni imamu wa Msikiti wa Zeinul Abedeen wa Kuwait amesema Mtume Mtukufu (saw) alitumwa na Mwenyezi Mungu ili aje kukamilisha misingi ya thamani na fadhila za kimaadili na kiakhlaqi na kwamba Waislamu wanapasa kuwadhihirishia sura halisi ya Uislamu wafuasia wa dini nyinginezo kwa kulinda umoja na mshikamano miongoni mwao. 678260
captcha