Karii wa Qur'ani wa Uingereza anayeshiriki katika Mashindano ya Tatu ya Qur'ani ya Wanachuo Waislamu nchini Iran amesema kuwa anaamini suala muhimu na la kwanza kwa karii na msomaji Qur'ani ni kujisabilia na kujitoa wakfu kwa ajili ya kitabu hicho kitakatifu na kutafuta muradi wake katika aya za kitabu hicho cha Mwenyezi Mungu.
Muhammad Ayyub Asif ameliambia shirika la habari la IQNA kwamba watu waliopewa sauti nzuri na Mwenyezi Mungu wametunukiwa neema kubwa na itakuwa bora zaidi iwapo neema hiyo itatumiwa katika kusoma Qur'ani Tukufu.
Muhammad Ayyub Asif ambaye kwa sasa ni mwanafunzi katika Chuo Kikuu cha al Azhar nchini Misri amesema kuwa alianza kujifunza Qur'ani Tukufu akiwa na umri wa miaka mitano. Anasema kuwa daima alikuwa na hamu ya kuweza kusoma Qur'ani kama makarii mashuhuri wa Qur'ani katika ulimwengu wa Kiislamu.
Anasema makarii anaowafadhilisha zaidi ni Mustafa Ismail, Khalil al Khisari na Muhammad Rif'at.
Amewausia wanafunzi wa rika lake kufanya jitihada za kukifahamu vyema kitabu cha Qur'ani Tukufu ambacho amesisitiza kuwa kiliteremshwa kwa ajili ya saada na ufanisi wa mwanadamu. 700042