IQNA

Askari wa Israel wawashambulia Wapalestina katika Msikiti wa Al Aqsa

22:25 - January 31, 2020
Habari ID: 3472423
TEHRAN (IQNA) - Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wameuhujumu Msikiti wa Al Aqsa katika mji wa Quds (Jerusalem) unaokaliwa kwa mabavu na utawala huo na kuwajeruhi Wapalestina kadhaa waliokuwa wamefika hapo kwa ajili ya Sala ya Ijumaa.

Kwa mujibu duru za habari, maelfu ya Wapalestina leo Ijumaa walifika katika Msikiti wa Al Aqsa kwa lengo la kushiriki katika Sala ya Ijumaa.

Wapalestina wameitaja Ijumaa ya leo kuwa 'Ijumaa ya Hasira' kama njia ya kubainisha upinzani wao kwa mpango wa kibaguzi wa Rais Trump wa Marekani uliopewa jina la 'Muamala wa Karne' kuhusu utatuzi wa kadhia ya Palestina. Walioshiriki katika sala hiyo ya Ijumaa walisikika wakitoa nara ya 'Naitoa nafsi yangu muhanga kwa ajili ya Msikiti wa Al Aqsa' wakati wakiingia katika eneo hilo takatifu.

Taarifa zinasema makumi ya Wapalestina wamejeruhiwa wakati wanajeshi wa utawala wa Kizayuni waliopowahujumu waumini huku wengine wakikamatwa.

Ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu zimeshuhudia maandamano makubwa ya Wapalestina wanaopinga mpango wa 'muamala wa karne' wa rais wa Marekani ambao unaunga mkono utawala ghasibu wa Israel na kukandamiza kikamilifu haki za taifa la Palestina. Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wanatumia nguvu za ziada kukabiliana na Wapalestina wanaoandamana.

Mpango wa Muamala wa Karne uliopendekezwa na Marekani unajumuisha kukabidhiwa kikamilifu Israel mji mtakatifu wa Quds wenye Kibla cha Kwanza cha Waislamu yaani Msikiti wa al Aqsa, vitongoji vilivyoko katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan vyote ipewe Israel, Wapalestina wasiwe na haki ya kurejea kwenye ardhi za mababu zao na makundi ya muqawama wa Palestina yapokonywe silaha ili kusiwe na jambo lolote linalohatarisha usalama wa utawala wa Kizayuni wa Israel.

Siku ya Jumanne, rais wa Marekani, Donald Trump alizindua mpango huo akiwa pamoja na waziri mkuu wa utawala wa Kizayuni, Benjamin Netanyahu. Trump alizindua mpango huo wa kidhulma baada ya kufanya mazungumzo pia na Benny Gantz, mkuu wa Muungano wa Blu na Nyeupe wa utawala pandikizi ambaye ni mpinzani mkuu wa Benjamin Netanyahu katika siasa za hivi sasa za Israel.

/3875336

captcha