IQNA

Indonesia yatangaza raia wake hawataenda Hija mwaka huu kutokana na COVID-19

17:49 - June 02, 2020
Habari ID: 3472827
TEHRAN (IQNA) – Serikali ya Indonesia imesema raia wa nchi hiyo mwaka huu hawataweza kutekeleza Ibada ya Hija kutokana na hofu ya maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19 au corona.

Waziri wa Masuala ya Kidini Indonesia Fachrul Razi ametangaza rasmi Jumanne kuwa, safari zote za Hija za raia wa Indonesia zimefutwa mwaka huu.

"Serikali imeamua kufuta Ibada ya Hija mwaka wa 2020 baada ya wakuu wa Saudi Arabia kushindwa kutangaza kwa yakini msimamo wao," amesema Facrul Razi alipozungumza na waandishi habari mjini Jakarta.

Waziri huyo amesema uamuzi huo umechukuliwa baada ya uzingatiaji wa kina hasa kuhusu masuala ya kiafya. Aidha Facrul Razi ameelezea matumaini yake kuwa Hija itaweza kufanyika mwaka ujao, Inshallah.

Indonesia ambayo ni nchi yenye idadi kubwa zaidi ya Waislamu duniani pia hupelekea idadi kubwa zaidi ya Mahujaji ambapo mwaka huu ilitazamiwa kupeleka raia wake wapatao 221, 000 kutekeleza ibada ya Hija nchini Saudia.

Mwezi Machi Waziri wa Hija wa Saudi Arabia aliwataka Waislamu kote duniani kusitiha kwa muda maandalizi ya ibada ya mwaka huu ya Hija hadi pale hali ya mambo kuhusiana na maambukizi ya virusi vya corona duniani itakapobainika vyema.

Waziri wa Hija wa Saudi Arabia ,Mohammed Saleh Benten amesema, katika mahojiano na televisheni amesema, kwa kuzingatia hali ya sasa ya janga la ugonjwa wa COVID-19 au corona na kwa kutilia maanani kuwa suala la afya ya mahujaji linapewa umuhimu; Saudia inawaomba Waislamu katika nchi zote kusubiri kabla ya kufanya maandalizi ya Hija hadi pale hali itakapoboreka.

Tayari Saudia imeshafuta safari zote za Umrah kwa karibu muda wa miezi miwili iliyopita kutokana na janga la COVID-19.

3471587

captcha