Waziri wa Hija wa Saudi Arabia ,Mohammed Saleh Benten amesema, katika mahojiano na televisheni amesema, kwa kuzingatia hali ya sasa ya janga la ugonjwa wa COVID-19 au corona na kwa kutilia maanani kuwa suala la afya ya mahujaji linapewa umuhimu; Saudia inawaomba Waislamu katika nchi zote kusubiri kabla ya kufanya maandalizi ya Hija hadi pale hali itakapoboreka.
Waziri wa Hija wa Saudia ameongeza kuwa kwa sasa nchi hiyo inafanya jitihada za kuwarejesha makwao karibu waumini 1,200 waliokwenda Makka kwa ajili ya ibada ya Umrah baada ya nchi zao kufunga viwanja vya ndege kutokana na maambukizi ya virusi vya corona.
Tarehe 18 mwezi uliopita wa Machi Saudi Araba ilipiga marufuku ibada ya Swala katika misikiti miwili mitakatifu zaidi ya Makka na Madina kwa hofu ya maambukizi ya virusi vya corona na imesimamisha ibada ya Umrah kwa Waislamu wote.
Zaidi ya watu 1, 500 wameambukizwa virusi vya corona nchini Saudi Arabia na 10 miongoni mwao wameripotiwa kufariki dunia.
Karibu Waislamu milioni tatu hutekeleza ibada ya Hija kila mwaka nchini Saudi Arabia na mwaka huu kuna hofu ya kutotekelezwa ibada hiyo ambayo ni nguzo ya Uislamu kutokana na hofu ya kuenea ugonjwa wa corona. Nchi nyingi duniani zimepiga marufuku safari za ndege za kimataifa kwa muda usiojulikana.