Amr Musa, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ametangaza habari ya kufanyika kikao cha dharura cha Mawaziri wa Mambo ya Nje wanachama wa jumuiya hiyo siku ya Ijumaa wiki hii nchini Kuwait, kwa ajili ya kufanya mashauriano kuhusiana na mgogoro wa Ukanda wa Gaza huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu na utawala ghasibu wa Israel.
Amesema, kikao hicho kinafanyika kutokana na ombi la Qatar kwa ajili ya kuchunguza mashambulio ya kinyama yanayotekelezwa na utawala haramu wa Israel dhidi ya watu wasio na hatia katika ukanda huo.
Amr Musa ameashiria upuuzaji wa utawala haramu wa Israel wa sheria za kimataifa na azimio la hivi karibuni la Baraza la Usalama la kuutaka usimamishe haraka mashambulio yake huko Gaza na kusema kuwa, hali ya kibinadamu katika ukanda huo ni ya kusikitisha na kutisha mno. Amezitaka jumuiya na mashirika ya kimataifa kuchukua hatua za haraka ili kukabiliana na hali hiyo. Amedai kwamba Jumuiya ya Nchi za Kiarabu imefanya juhudi zake zote kwa ajili ya kusimamisha mashambulio hayo ya kinyama na pia kuwapelekea wakazi wa ukanda huo misaada ya dharura ya kibinadamu. 347435