Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran yaani Bunge amesema kuwa, njama na fitina zote zitakazofanywa na maadui dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran zitafeli kutokana na tadbiri ya Kiongozi Mudhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Akihutubia mbele ya halaiki ya wananchi wa Mkoa wa Mazandaran kaskazini mwa Iran, Dakta Ali Larijani ameongeza kuwa, Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran yamekumbwa na misukosuko mingi na kusisitiza kuwa, mirengo kadhaa ya kisiasa haina uelewa wa kutosha juu ya umahiri wa Mapinduzi ya Kiislamu na imejikuta ikitumbukia kwenye uanzishaji wa fitina za ndani kutokana na uchochezi wa Marekani na nchi za Magharibi.
Huku akieleza kuwa utawala fakihi ndiyo mhimili na nguzo muhimu katika kuendesha mambo mengi nchini ameongeza kuwa, nchi za Magharibi zimetumia mbinu mbalimbali kwa minajili ya kuzusha fitina na mifarakano kati ya wananchi wa Iran ili ziweze kufikia malengo yao haramu, lakini kwamba licha ya njama zote hizo utawala wa fakihi umesimama imara bila ya kutetereka katika kuzima njama hizo.
803719