IQNA

Onyo dhidi ya kuuzwa Qur'ani zilizo na kasoro za chapa mjini Makka na Madina

10:35 - August 19, 2011
Habari ID: 2173066
Naibu Waziri anayesimamia masuala ya magazeti na utafiti wa kielimu katika Wizara ya Wakfu ya Saudi Arabia ametahadharisha dhidi ya kuuzwa Qur'ani Tukufu zilizo na kasoro za chapa katika maktaba na maduka ya vitabu katika miji mitakatifu ya Makka na Madina.
Naibu Waziri Musaid al-Hadithi amesema kuwa nakala kadhaa zilizo na makosa makubwa ya chapa zinaendelea kuuzwa katika miji hiyo mitakatifu. Naibu Waziri huyo amesema kwamba nyingi ya nuskha hizo huwachwa katika misikiti miwili mitukufu ya Haram na wa Mtume mjini Madina na Waislamu wanaofanya ibada ya umra, ambao wengi amedai wanatoka katika nchi za Syria na Lebanon. Ametaka kukusanywa kwa nakala hizo mara moja.
Musaid al-Hadithi amesema nakala hizo huchapishwa na mashirika ambayo sio ya Kiislamu ambayo lengo lao kuu ni kunufaika kibiashara na kujiwekea mfukoni faida nono za kifedha.
Amesikitishwa sana na hali ya kuwa tatizo hilo limetokea katika mwezi mtukufu wa Ramadhani ambao ni mwezi ilioteremshwa ndani yake kitabu hicho kitakatifu.
Hata hivyo amesema kuwa hiyo si mara ya kwanza kwa tatizo kama hilo kujitokeza kwa sababu hivi karibuni pia nuskha kama hizo zilizo na kasoro ya chapa zilizochapishiwa nchini China zilipatikana katika maeneo hayo matakatifu. 845158
captcha