Ofisi ya askofu mkuu wa Kanisa la Makhufti wa Misri imesema kuwa ni jinai kubwa kuvunjia heshima matukufu ya kidini na kwamba ni jambo lisilokubalika na kila mtu anayeheshimu mafundisho ya kidini.
Ofisi hiyo imesema kwamba uvunjiwaji heshima matukufu ya kidini utazidisha tu hitilafu kati ya wafuasi wa dini mbalimbali. Imesisitiza udharura wa kuheshimiwa misingi na thamani za kimaanawi pamoja na kuimarishwa mazungumzo ya kuvumiliana wafuasi wa dini tofauti.
Kanisa la Makhufti wa Misri au kwa jina jingine Makopti, limepinga vikali kila aina ya uvamizi na ukaliwaji wa mabavu wa ardhi za mataifa mengine ukiwemo uvamizi wa Marekani nchini Afghanistan na utawala ghasibu wa Israel katika ardhi za Palestina.
Ofisi hiyo imeutaka Umoja wa Mataifa kufanya juhudi za kukomesha uvamizi wa nchi mbili hizo ambao imesema ndicho chanzo cha migogoro muhimu ya kidini duniani.
Vilevile imewataka wafuasi walio na misimamo ya wastani wa dini zote duniani kupambana na hatua kama hizo za uvamizi zinazochochea hisia za Waislamu. Imesema kuheshimiwa itikadi za watu wengine na matukufu yao ni sehemu muhimu ya imani ya waumini wa dini tofauti za mbinguni. 961971