Kongamano hilo lilimaliza shughuli zake usiku wa jana Jumapili ambapo kulisisitizwa kuwa, hitilafu za kisiasa hazipaswi kuzusha mgawanyiko kati ya safu ya umma wa Kiislamu hasa katika uga wa kiitikadi, kihistoria na kifiq’hi, kwani kuzuka fitina za kimadhehebu na ubaguzi ni kwa manufaa ya maadui wa umma huu
Katika ripoti hiyo, sambamba na kulaani kila aina ya jinai za utawala haramu wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina, kwa mara nyingine kumesisitizwa juu ya udharura wa kutekelezwa haki za kisheria za taifa madhlumu la Palestina huku suala muhimu likiwa ni kuainishwa mustakbali na kuundwa taifa huru la Palestina mji mku wake ukiwa Baytul-Muqaddas sanjari na kurejea wakimbizi wa Kipalestina. Aidha mwishoni mwa kongamano hilo la Kimataifa la Umoja wa Kiislamu, washiriki wamesisitizia juu ya kulindwa heshima kati ya Waislamu na kuacha kadhia zenye hitilafu kwa maulama na wataalamu sambamba na kutovunjiwa heshima na kudharauliwa shakhsia wa kidini. Kuhusiana na hilo, washiriki wameunga mkono fatuwa ya kihistoria ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Sayyid Ali Khamenei inayoharamisha kuvunjiwa heshima shakhsia wa madhehebu za Kiislamu na kuwakejeli wake za Mtukufu Mtume Muhammad (saw).
1360694