IQNA

Hukumu Dhidi ya Mchoma Qur'ani Yabatilishwa Uingereza kwa Kisingizio cha ‘Uhuru wa Maoni’

19:29 - October 11, 2025
Habari ID: 3481354
IQNA – Hukumu dhidi ya mwanaume aliyepigwa faini kwa kuchoma nakala ya Qur'an nje ya ubalozi wa Uturuki jijini London imebatilishwa kwa kisingizio cha eti “uhuru wa kujieleza.”

Hamit Coskun, mwenye umri wa miaka 51, alisikika akitoa matusi dhidi ya Uislamu huku akiinua kitabu kitakatifu kilichokuwa kinawaka moto katika eneo la Rutland Gardens, Knightsbridge, mnamo tarehe 13 Februari.

Mnamo mwezi Juni, alikutwa na hatia katika Mahakama ya Westminster kwa kosa la kuharibu utaratibu wa umma kwa misingi ya chuki ya kidini, na akapigwa faini ya pauni 240.

Hata hivyo, katika Mahakama ya Southwark Crown siku ya Ijumaa, Jaji Bennathan alisema kuwa ingawa kuchoma Qur'an ni jambo “linalowaumiza na kuwakwaza Waislamu wengi kwa kiwango kikubwa,” haki ya kujieleza “inapaswa kujumuisha haki ya kutoa maoni yanayokera, kushangaza au kusumbua.”

Jaji huyo aliongeza: “Tunaishi katika demokrasia huria. Moja ya haki adhimu tunazopewa ni uwezo wa kutoa maoni yetu binafsi na kusoma, kusikiliza na kutafakari mawazo bila serikali kuingilia kati kutuzuia kufanya hivyo. Gharama ya haki hiyo ni kuwaruhusu wengine pia kutumia haki hizo, hata kama yanayotamkwa yanatuumiza au kutukera.”

Sheria za kukemea matusi dhidi ya dini (blasphemy) zilifutwa rasmi nchini England na Wales mwaka 2008, na nchini Scotland mwaka 2021.

3494949

captcha