Akizungumza leo Jumanne asubuhi hapa Tehran mbele ya hadhara ya wageni kutoka nchi mbalimbali duniani wanaokuja kushiriki maadhimisho ya kutimia 25 ya kufariki dunia Imam Khomeini, Rais Rouhani ameongeza kuwa, Imam alianzisha harakati kubwa ya Kiislamu yapata miaka 50 iliyopita. Rais Rouhani ameongeza kuwa, hakuna mtu yeyote aliyefikiri na kutasawari kwamba katika kipindi kifupi tu Imam angeliweza kukabiliana na matatizo yote ya ndani na kimataifa na hatimaye kujipatia ushindi adhimu. Rais wa Iran amesema kuwa, katika kipindi cha miongo mitano iliyopita, Iran ilikuwa chini ya ukandamizaji wa madola ya kibeberu na kusisitiza kwamba wananchi wa Iran wenye uzoefu wa ustaarabu wa maelfu ya miaka waliupokea Uislamu baada ya kubaathiwa na kupewa utume Mtume Muhammad SAW. Ameongeza kuwa, Iran ilikuwa na nafasi muhimu katika ustawi wa utamaduni na ustaarabu wa Kiislamu, lakini inasikitisha kuona kwamba katika karne za hivi karibuni haikuwa na nafasi yoyote kiutawala. Rais Rouhani ameongeza kuwa, madola ya kibeberu na hasa Uingereza na Marekani yalikuwa yakiingilia masuala ya ndani ya Iran na katika masuala muhimu na nyeti ya kitaifa hapa nchini, na kuyatolea maamuzi bila ya ridhaa ya wananchi, lakini Imam Khomeini alisimama kidete na kukabiliana na madola hayo ya kibeberu duniani. Imeelezwa kuwa, jumla ya shakhsia 400 wa kiutamaduni, kidini , kisiasa na wahadhiri kutoka nchi 29 duniani wako hapa nchini kwa lengo la kushiriki kwenye maadhimisho hayo.