
Katika hafla rasmi, Sheikh Ahmed Awad Abu Fayouz alimkabidhi Sheikh Ghalban cheti maalum cha kuthamini mchango wake mkubwa katika kuhudumia Qur'ani na kueneza elimu zake. Tukio hili ni sehemu ya juhudi za umoja huo kuwatambua na kuwaheshimu mashujaa wa Qur'ani waliotumia maisha yao katika kuitumikia Qur'ani Tukufu na kufundisha usomaji wake kwa ufasaha.
Sheikh Ghalban amekuwa na mchango mkubwa katika kufundisha kanuni za Tajweed na adabu za usomaji wa Qur'ani, akilea vizazi vya maqarī na wahifadhi wa Qur'an ndani ya Kafr el-Sheikh na maeneo mengine. Anatambulika kama mwanachuoni wa Al-Azhar aliyejikita kikamilifu katika jukumu lake la kuhudumia Kitabu Kitakatifu.
Sheikh Fayouz alieleza katika hafla hiyo kuwa, umoja wao daima umejitahidi kutambua juhudi za wanachuoni na wasomaji wa Qur'ani waliotoa mchango wa dhahiri katika kuitumikia Qur'ani Tukufu. Aliongeza kuwa Sheikh Ghalban ni miongoni mwa wasomaji mahiri, wenye adabu, unyenyekevu na moyo wa kutoa. Sheikh Ghalban alishukuru umoja huo kwa hatua hiyo ya thamani, akisisitiza kuwa kuitumikia Qur'ani ni heshima kubwa na neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu kabla ya kuwa ni kutoka kwa watu. Sheikh Ghalban alizaliwa Machi 26, 1946 katika mji wa Desouq, mkoa wa Kafr el-Sheikh.
Alijifunza mitindo saba ya usomaji wa Qur'ani kutoka kwa Sheikh al-Fadli Ali Abu Layla ndani ya Msikiti wa Ibrahim Al-Desouqi ulioko mji wake wa asili. Kwa sasa, Sheikh Ghalban anaongoza mduara wa usomaji wa Qur'an katika mji wa Desouq. Misri ni nchi ya Afrika Kaskazini yenye idadi ya watu takriban milioni 115. Takwimu rasmi zinaonesha kuwa karibu asilimia 90 ya wakazi wake ni Waislamu. Shughuli za Qur'ani ni jambo la kawaida na lenye hadhi kubwa katika taifa hili la Waarabu lenye Waislamu wengi, ambapo maqarī mashuhuri wa ulimwengu wa Kiislamu, wa zamani na wa sasa, wengi wao wametoka Misri. /3495206