Ehud Barak amesema kuwa, wanasubiri matokeo ya uchaguzi wa rais wa Misri na kwamba wanamtaka rais atakayeshinda uchaguzi huo aheshimu mkataba wa Camp David.
Duru ya pili ya uchaguzi wa Rais wa Misri ilimalizika jana kati ya mgombea wa Ikhwanul Muslimin Muhammad Morsi na Ahmad Shafiq Waziri Mkuu wa mwisho wa utawala wa Hosni Mubarak uliopinduliwa na mapinduzi ya wananchi.
Katika kampezi zao za uchaguzi Shafiq aliahidi kuendelea kuheshimu mkataba huo uliotiwa saini mwaka 1978 kati ya Misri na Israel lakini Morsi amesema kuwa atavunja makubaliano hayo.
Waziri wa Vita wa Israel ameashiria kuuawa watu wanne katika mapigano kwenye mpaka wa ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Israel na Misri na kudai kuwa, serikali ya Cairo haiwezi kudhibiti usalama wa nchi na kuitaka nchi hiyo kushirikiana na Tel Aviv katika kuimarisha usalama wa mpakani.
Wakati hayo yakiripotiwa taarifa zinasema kuwa Israel imepeleka vifaru katika mpaka wa kusini wa ardhi unazozikalia kwa mabavu za Palestina na Misri, hatua ambayo ni kinyume na mkataba wa Camp David.
1031710