IQNA – Siku ya Kimataifa ya Usomaji wa Qur’ani itaadhimishwa baadaye mwezi huu chini ya usimamizi wa Kituo cha Kiislamu cha Al-Azhar nchini Misri.
Al-Azhar inaandaa shughuli mbalimbali za kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Usomaji wa Qur’ani mnamo Agosti 30, kwa lengo la kusoma Qur’ani nzima au sehemu zake ndani ya siku moja.
Tukio hili ni mpango wa kila mwaka, ambapo toleo lake la mwisho lilishuhudia ushiriki wa zaidi ya watu 100,000 kutoka Misri na maelfu wengine kutoka nje ya nchi hiyo.
Taasisi mbalimbali, zikiwemo vituo vya kuhifadhi Qur’ani vinavyoshirikiana na Al-Azhar, taasisi za kiserikali, Jumuiya ya Kimataifa ya Wahitimu wa Al-Azhar, Jukwaa la Utafiti wa Kiislamu la Misri, Chuo Kikuu cha Al-Azhar, na Kurugenzi Kuu ya Shule za Chekechea, pamoja na vituo na watu kutoka duniani kote, hushiriki katika programu za siku hii.
Tukio hili si usomaji wa Qur’ani wa siku moja tu; bali ni jaribio la kivitendo la kupima kiwango cha uimarishaji wa hifdhi, uwezo wa kukumbuka aya, na uwezo wa kusoma mfululizo. Inampa kila mshiriki fursa ya kushuhudia matunda ya juhudi zao za Qur’ani na kufikia hatua ya umahiri katika hatua za kuhifadhi na kurudia aya.
Tukio hili lina sehemu mbili: ‘Usomaji Kamili’ ambapo Hafidh husoma Qur’ani nzima kwa kumbukumbu mbele ya mwalimu wa Qur’ani au mwenzake ndani ya siku moja, na ‘Usomaji wa Sehemu’ ambao unaruhusu washiriki kusoma sehemu yoyote ya Qur’ani wanayoweza. Hii, kama njia ya kufundishia kupitia mazoezi endelevu na urudiaji, huwaandaa washiriki kufikia hatua ya kusoma Qur’ani nzima.
“Iqra wa Irtaq: Soma na Upae” ndiyo kaulimbiu ya Siku ya Kimataifa ya Usomaji wa Qur’ani, na ni ujumbe kwa wale wote ambao wameifanya Qur’ani kuwa mwenza katika njia yao ya maisha.
3498685