Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, Ayatullah Mohammad Yazdi ambaye alikuwa amelazwa hospitalini, ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 89.
Hadi wakati wa kifo chake, Ayatullah Mohammad Yazdi, alikuwa mwenyekiti wa Jumuiya ya Wasomi na Wahadhiri wa Chuo cha Kidini cha Qum na pia mwanachama wa Baraza la Wanazuoni Wataalamu Wanaomchagua Kiongozi Muadhamu.
Mwanazuoni huyo, ambaye alitumia umri wake uliojaa baraka katika jihadi kwa njia ya Uislamu, aliwahi kuwa mkuu wa Idara ya Mahakama ya Iran kwa muda wa miaka 10. Aidha aliwahi pia kuwa mwenyekiti wa Baraza la Wanazuoni Wataalamu Wanaomchagua Kiongozi Muadhamu kati ya nyadhifa zingine muhimu.
Mwanazuoni huyu mwanajihadi ameandika vitabu kadhaa na makala nyingi katika nyuga mbali mbali za Kiislamu.
Ayatullah Muhammad Yazdi atakumbukwa kwa ushujaa wake pamoja na ujasiri wake katika kutetea malengo matukufu ya Mapinduzi ya Kiislamu. Viongozi mbali mbali wa Iran wanaendelea kutuma salamu za rambi rambi kufuatia kuaga dunia mwanazuoni huyo.