IQNA

11:47 - December 21, 2008
Habari ID: 1720981

Wanachuo wa ulimwengu wa Kiislamu waziamshe serikali za Kiarabu kuhusu maafa ya Gaza

Imeelezwa kwamba katika kipindi cha sasa kuna udharura wa nchi za Kiislamu na Kiarabu kushikama katika kutafuta suluhisho la Palestina na kuchukua hatua za haraka za kimataifa kuhusu kadhia hiyo. Hata hivyo inasikitisha kwamba serikali za Kiarabu zimelala fofofo na kusahau maafa yanayowasibu wakazi wa Ukanda wa Gaza.

Katika hali hiyo ni wanafunzi wa vyuo vikuu vya ulimwengu wa Kiislamu ambao wanapaswa kuwaamsha viongozi wasiokuwa na ghera wa nchi hizo.
Hayo yamesemwa katika taarifa ya Jumuiya ya Kiislamu ya Wanafunzi wa Vyuo Vikuu vya Iran (SADA). Jumuiya hiyo imempongeza mwandishi habari Muiraqi Muntadhir Zaydi aliyempopoa kwa viatu Rais George Bush wa Marekani na kulaani jinai zinazofanywa na utawala ghasibu wa Israel huko Gaza. Jumuiya ya SADA imeitaka Jumuiya ya Nchi za Kiislamu (OIC) na Jumuiya ya Nchi Zisizofungamana na Siasa za Upande Wowote (NAM) kuitisha mkutano wa dharura kujadili kadhia hiyo.
Taarifa hiyo imesema: Kitendo cha mwandishi habari shujaa Muntadhir Zaydi cha kudhihirisha chuki ya wananchi Waislamu wa Iraq dhidi ya wavamizi wa Kimarekani na kumshambulia Bush kwa viatu si harakati ya mtu binafsi bali ni dhihirisho la hasira na chuki ya taifa la Iraq dhidi ya wavamizi waliochezea shere uhuru na utu wa wananchi wa Iraq katika kipindi chote cha kukaliwa kwa mabavu nchi yao. Taarifa hiyo imesisitiza kwamba harakti hiyo inapaswa kupongezwa na watu wote huru.
Taarifa ya Jumuiya ya Kiislamu ya Wanafunzi wa Vyuo Vikuu nchini Iran imeashiria hali mbaya na maafa ya wakazi milioni moja na nusu wa Ukanda wa Gaza na kuzilaumu jumuiya za kimataifa hususan Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa kuendelea kunyamaza kimya mbele ya jinai hizo. 335660
captcha