Tovuti ya lecfcm imeripoti kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Waislamu wa Ufaransa Muhammad Mussawi amelaani shambulizi la kigaidi lililotokea karibu na kanisa moja mjini Alexandria nchini Misri na kusisitiza kwamba ni kitendo cha kinyama.
Taarifa ya CFCM imeongeza kuwa Baraza la Waislamu wa Ufaransa linasikitishwa mno na tukio hilo lililotokea sambamba na kuanza mwaka mpya wa Miladia na linawataka watu wote huru na watetezi wa amani duniani kusimama katika safu moja kwa ajili ya kupambana na dhulma na ugaidi.
Katika sehemu nyingine ya taarifa hiyo, Muhammad Mussawi ametoa rambirambi kwa familia za watu waliopoteza maisha yao kwenye mashambulizi hayo ya kigaidi, serikali na wananchi wa Misri na amewataka Wamisri kuungana na kutilia maanani udugu wa kidini kwa ajili ya kuzima njama hizo zinazolenga kuzusha hitilafu kati ya Waislamu na Wakristo. 722465