Mpango huo wa Wazayuni ni katika fremu ya kujenga vitongoji vingine 6,000 katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.
Kwa mujibu wa tovuti ya Kizayuni ya Yedioth Ahronoth, nyumba hizo 1,028 zitajengwa katika vitongoji vitatu katika miji inayokaliwa kwa mabavu ya Quds na Beitlahm.
Hayo yanajiri katika hali ambayo nchi kadhaa wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC) zimekosoa hatua ya Israel ya kupanua na kuendeleza ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi za Palestina inazozikalia kwa mabavu na kushadidi pia mashambulizi ya walowezi hao dhidi ya raia wa Palestina.
Ufaransa, Uingereza, Ujerumani na Ureno zimesema katika taarifa yao ya pamoja baada ya kikao hicho cha Baraza la Usalama kuhusiana na mgogoro wa Mashariki ya Kati hapo jana kuwa zinatiwa hofu na vitendo hivyo hasi vya utawala wa Kizayuni vinavyotishia amani katika eneo la Mashariki ya Kati.
Nchi hizo nne za Umoja wa Ulaya zimelaani pia athari kubwa zinazosababishwa na uendelezaji wa ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Ufaransa, Uingereza, Ujerumani na Ureno pia zimeitaka Tel Aviv kuchukua hatua kali za kusimamisha mashambulizi ya walowezi wa Kiyahudi dhidi ya raia wa Palestina na misikiti yao.