IQNA

18:03 - August 17, 2026
Habari ID: 3482637

Baraza la Kimataifa la Qur’an laanzishwa mjini Istanbul, Uturuki

IQNA – Maafisa wa Maonyesho ya 11 ya Kimataifa ya Vitabu ya Istanbul wametangaza kuanzishwa kwa “Baraza la Kimataifa la Qur’an” (World Quran Assembly) pembezoni mwa siku ya kwanza ya hafla hiyo.

Baraza la Qurani

Maonyesho ya 11 ya Kimataifa ya Vitabu cha Kiarabu ya Istanbul yalifunguliwa Jumamosi jijini Istanbul na yataendelea hadi Agosti 23, yakibeba kaulimbiu ya “Hadithi Inaendelea”.

Katika siku ya kwanza ya maonyesho hayo, kundi la wasomi kutoka ulimwengu wa Kiislamu lilitangaza rasmi kuzinduliwa kwa Baraza la Kimataifa la Qur’an.

Taarifa iliyotolewa na bodi ya waanzilishi wa baraza hilo katika mkutano maalum ilisema: “Leo, tunatangaza kuzinduliwa kwa Baraza la Kimataifa la Qur’an na ufunguzi wa jukwaa la usajili kwa ajili ya taasisi, vituo, duru za usomaji (halaqa), na akademia za Qur’an duniani kote.”

Taarifa hiyo iliongeza: “Tangazo la kuanzishwa kwa baraza hili jijini Istanbul ni wakati wa kihistoria katika maendeleo ya shughuli za kitaasisi za Qur’an, na wazo hili lilianzia katika viwanja vya Msikiti wa Al-Aqsa na Al-Quds Tukufu.”

Taarifa hiyo ilibainisha kuwa wazo hilo lilianza kwa swali rahisi lakini lenye kina: Je, ingekuwaje kama watu wa Qur’an duniani wangefahamiana? Je, ingekuwaje kama maelfu ya taasisi,  zote zikihudumia kitabu kimoja na kuwa na ujumbe mmoja, lakini mara nyingi zikiwa hazijui uwepo wa kila mmoja,  zingekutana pamoja? Je, ingekuwaje kama uzoefu uliotawanyika ungekuwa nguvu ya pamoja, mipango binafsi ikawa miradi ya kimataifa, na nguvu zilizotawanyika zikawa mtandao mmoja ulioungana unaofanya kazi kwa ushirikiano ili kulihudumia Kitabu cha Mwenyezi Mungu?

Ikibainisha kuwa wazo hilo lilipokelewa vizuri lilipowasilishwa kwa wasomi, wasomaji wa Qur’an (maqari), na taasisi mbalimbali, ilisisitizwa kuwa Baraza la Kimataifa la Qur’an lilianzishwa si kwa ajili ya kuwa “taasisi kuu” , wala kama mshindani au mbadala , bali kama mwavuli wa kimataifa.

Lengo lake ni kuhudumia na kuimarisha taasisi za Qur’an, kuhifadhi uhuru na utambulisho wao wa kipekee, na kufungua milango ya ushirikiano na ubia, ilisema taarifa hiyo.

Bodi ya waanzilishi wa baraza hilo inajumuisha kundi la wasomi mashuhuri, wasomaji wa Qur’an, na wasomi kutoka nchi mbalimbali duniani.

Sheikh Ahmed Issa Al-Masrawi kutoka Misri ndiye Rais wa baraza hilo, wakati Sheikh Abdul Rashid Sufi kutoka Qatar akiwa Makamu wa Rais, na Sheikh Ahmed Shukri Shabsugh kutoka Jordan akiwa Katibu.

Aidha, wasomi wa Qur’an wakiwemo Sheikh Abdul Salam Majidi (Yemen), Muhammad Amin Mashali (Uturuki), Ghanem Qaddouri Al-Hamd (Iraq), Kamal Qadeh (Algeria), Ahmed Mian Al-Tahnawi (Pakistan), Khairuddin Khoja (Kosovo), Abdul Rahman Al-Jamal (Palestina), Muhammad Ayden (Uturuki), Muhammad Zaytun Rasmin (Indonesia), Yahya Al-Ghouthani (Syria), Abdul Fattah Al-Farisi (Morocco), Muhammad Al-Hassan Bousso (Senegal), Hisham Abdul Bari Al-Rajh (Malaysia), Mustafa Ahmed Arafa (Kuwait), Hassan Muhammad Saleh (Marekani), na Ahmed Al-Sanami (Italia) ni wanachama waanzilishi wa baraza hili la Qur’an.

3498673

Habari zinazohusiana
captcha