Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Habari za Qur'ani IQNA, hayo yanajiri baada ya mafanikio ya Shirika la Bima la Takaful Afrika ambalo lilianzishwa mwaka 2011 likiwa shirika la kwanza kabisa linaloendesha shughuli zake kwa mujibu wa sheria za Kiislamu nchini Kenya.
Wakuu wa shirika la bima la Kenya Re-Insurance wanasema shirika hilo limeeneza wigo wake Afrika Magharibi na Mashariki ya kati na hivyo, ‘sasa wakati umewadia kwa Shirika Kubwa la Bima ya Kiislamu kuanza shughuli zake Kenya. Wakuu wa Kenya Re-Insurance wanasema kutokana na ongezeko la huduma za kifedha za Kiislamu, huduma za bima ya Kiislamu pia zitapata wateja. Katika miaka ya hivi karibuni huduma za kifedha za Kiislamu zimeimarika nchini Kenya kwa kufunguliwa benki kadhaa za Kiislamu na vile vile benki za kawaida zenye kutoa huduma maalumu kwa mujibu wa sheria za Kiislamu.