IQNA

Juhudi za vijana wa Kiislamu za kuondoa chuki za kidini dhidi ya Uislamu Ujerumani

14:14 - November 06, 2008
Habari ID: 1705165
Kundi la vijana wa Kiislamu nchini Ujerumani limeanzisha kampeni ya kuweka michoro na picha za kuvutia za Kiislamu katika mavazi ikiwa ni katika harakati za kupunguza chuki za kidini dhidi ya Uislamu nchini humo.
IQNA imenukuu kituo cha World Bulletin kwamba mchoraji Muislamu anayeishi Ujerumani Malih Kisman amebuni mpango huo kwa shabaha ya kupunguza chuki za kidini zinazokua zaidi dhidi ya Waislamu.
Malih Kisman amekiambia kituo cha World Bulletin kwamba alipata fikra hiyo baada ya kuchapishwa vibonzo vilivyomvunjia heshima Mtume Muhammad SAW nchini Denmark. Amesema kuwa mtindo huo unaeneza ujumbe wa amani wa Uislamu na kwamba lengo la kuchapisha ujumbe na picha za kuvutia juu ya mavazi ni kuwafanya watu wajaribu kudadisi na kuchunguza dini ya Kiislamu. Amesema, kundi hilo lilianza shughuli hiyo mwezi wa Ramadhani wa mwaka jana na kwamba hadi sasa limepata maelfu ya wateja kutoka pembe mbalimbali duniani.
Akieleza sababu ya kuchapisha picha na michoro ya kuvutia katika mavazi, msaani huyo wa Kiislamu amesema, Uislamu umehimiza juu ya furaha na bashasha na kwamba Mtume Muhammad SAW alikuwa akiwahimiza Waislamu kuonyesha tabasamu. Alikuwa mcheshi na mwenye kuzungumza na watu kwa moyo mkunjufu. Malih Kisman amesema, inasikitisha kwamba Waislamu wamesahau ukweli huo kuhusu tabia njema za Mtume Muhammad SAW. 316341
captcha