IQNA

Serbia yajaribu kumkamata aliyewaua Waislamu Bosnia

11:51 - November 16, 2008
Habari ID: 1708671
Serikali ya Serbia imetangaza kuwa ingali inaendeleza jitihada za kumtia mbaroni mmoja kati ya wahusika wakuu katika mauaji ya kimbari ya Waislamu katika vita vya Bosnia.
Wakuu wa Serbia wamesema, watatoa zawadi ya Euro milioni moja kwa yeyote atakayetoa habari kuhusu maficho ya mtendai jinai huyo wa kivita.
Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA katika eneo la Balkan, Wasim Libaich mwakilishi wa kudumu wa serikali ya Serbia katika Mahakama ya Jinai za Kivita ya The Hague ametoa taarifa hiyo na kusisitiza kuwa: 'zawadi ya Euro milioni moja ingalipo na hakuna mabadiliko yoyote katika suala hilo. Serikali ya Serbia iko tayari kulipa Euro milioni moja kwa ajili ya kutiwa mbaroni mtenda jinai Jenerali Ratko Mladic' .
"Mtenda jinai huyu wa kivita anatuhumiwa kutekeleza mauaji ya kimbari katika vita vilivyojiri maeneo mbali mbali ya Bosnia na vile vile alitoa amri ya kuuawa kwa umati maelfu ya watoto na wanawake Waislamu wasio na hatia katika vita vya Bosnia", amesema mwakilishi wa kudumu wa serikali ya Serbia katika Mahakama ya Jinai za Kivita ya The Hague.
Wasim Libaich ameongeza kuwa, 'Jenerali huyu aliyekuwa kamanda wa jeshi la Waserbia wa Bosnia alienda mafichoni kuanzia mwaka wa 1995'. Ameendelea kusema kuwa serikali ya Serbia inakusudia kutoa ushirikiano kamili hadi pale mtenda jinai huyo wa kivita atakapofikishwa katika mahakama ya The Hague.
Itakumbukwa kuwa Aprili Mosi mwaka 2008, Slobodan Milosevic mtenda jinai wa kivita wa Bosnia alitiwa nguvuni huku katili mwenzake Radovan Karadzic akinaswa Julai 21 na kukabidhiwa kwenye mahakama ya The Hague. 320285


captcha