IQNA

Hizbullah yakosoa kimya cha Umoja wa Mataifa mbele ya jinai za Israel

10:37 - April 27, 2009
Habari ID: 1770391
Mwakilishi wa harakati ya Hizbullah katika Bunge la Lebanon amesema kuwa hadi sasa Umoja wa Mataifa haujachukua msimamo wa wazi na wa kishujaa wa kulaani jinai za utawala wa Kizayuni wa Israel na kwamba upuuzaji huo ni alama ya udhaifu wa taasisi hiyo ya kimataifa.
Hassan Fadhlullah pia amekosoa misimamo ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon dhidi ya Hizbullah na akasema: Umoja huo umekuwa na misimamo ya kupendelea upande mmoja na umepuuza jinai zinazofanywa na viongozi wa Israel na ugaidi wa utawala huo ghasibu.
Kuhusu matamshi yaliyotolewa na Ban Ki-moon dhidi ya Hizbullah, Hassan Fadhlullah amesema kuwa Ki-moon ameufanya Umoja wa Mataifa kuwa chombo cha kuhudumia maslahi na usalama wa Israel. Ameongeza kuwa kiongozi huyo amenyamazia kimya jinai za Israel dhidi ya wananchi wa Lebanon na Palestina na kwamba baadhi ya jinai hizo zinafanyika katika makao ya umoja huo.
Mwakilishi wa Hizbullah katika Bunge la Lebanon amesema kuwa wakati wa mauaji ya halaiki ya wakazi wa kijiji cha Kana huko kusini mwa Lebanon, Umoja wa Mataifa ulishindwa kuwatetea raia waliokimbilia kwenye makao ya umoja huo kutafuta amani, suala ambalo linadhihirisha udhaifu wa jumuiya hiyo ya kimataifa na kushindwa kwake kudhamini amani na usalama wa raia. 394755
captcha