Papa Shenouda III, Kiongozi wa Kanisa la Makopti wa Misri amewaomba radhi Waislamu wote wa dunia kutokana na matamshi ya dharau yaliyotolewa hivi karibuni na Kasisi al-Anba Bishoy, Katibu wa Jumuiya ya Kikristo ya Misri kuhusiana na Qur'ani.
Akizungumza hivi karibuni na televisheni ya Misri, Papa Shenouda amesema kuwa amesikitishwa mno na matamshi ya kasisi huyo ambayo yamewaudhi Waislamu. Amesema mjadala kuhusu itikadi za dini nyinginezo ni mstari mwekundu ambao haupaswi kuvukwa na kwamba kuchukua msimamo kuhusiana na suala hilo ni jambo linalopaswa kuepukwa. Amevitaka vyombo vya habari pia kutochochea suala hilo. Amedai kwamba vyombo vya habari havikuakisi vyema maneno ya Kasisi Bishoy kwa kusema kuwa alidai kuwa Waislamu nchini Misri ni wageni hali ya kuwa ukweli wa mambo ni kuwa Waislamu ndio walio wengi nchini humo.
Tunakumbusha hapa kuwa wiki iliyopita Kasisi Bishoy alidai huko Cyprus kwamba kuna aya ambayo iliongezwa kwenye Qur'ani Tukufu baada ya kuaga dunia Mtume (saw) na katika zama za utawala wa Khalifa Othman, jambo ambalo limeamsha hasira kubwa ya wanazuoni wa nchi za Kiislamu na hasa wa Misri. Makopti nchini Misri wanaunda asilimia 5 ya wananchi wa nchi hiyo. 663555