IQNA

Waislamu wa Ujerumani wakaribisha matamshi ya rais wa nchi hiyo

17:10 - October 05, 2010
Habari ID: 2007217
Ayman Mazyek, Katibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu wa Ujerumani amekaribisha matamshi ya Rais Christian Wulff wa nchi hiyo kuhusiana na suala la haki za Waislamu.
Akizungumza hivi karibuni na gazeti la Bild, Mazyek amesifu matamshi hayo ya Rais Wulff na kusema Waislamu wa nchi hiyo wanakaribisha uimarishwaji wa uhusiano wao na serikali ya Ujerumani. Amesema matamshi ya rais huyo yamethibitisha wazi kuwa Waislamu wa Ujerumani hawapasi kuchukuliwa kuwa raia wa daraja la pili nchini humo na kuwa hilo ni jambo la kutia moyo.
Katika sehemu nyingine ya matamshi yake, katibu mkuu huyo amesema Rais Wulff amesema wazi kwamba, tofauti za maisha ya mtu binafsi na ya kijamii ya watu mbalimbali ni jambo la kawaida na kwamba jambo hilo halipasi kukuzwa kuliko kiasi.
Tunakumbusha hapa kuwa katika hotuba yake ya hivi karibuni kwa mnasaba wa kuadhimishwa siku ya kubomolewa ukuta wa Berlin na kuungana Ujerumani mbili za Magharibi na Mashariki, Rais Wulff alisema kuwa Waislamu ni sehemu ya jamii ya Ujerumani na kwamba Wajerumani wote wanapasa kupewa haki sawa. 668629
captcha