Gazeti la Daily Telegraph linalochapishwa Uingereza, limechambua kwa kina suala la ushindi wa vyama vya Kiislamu katika nchi ambazo zinashuhudia wimbi la mwamko wa Kiislamu na hasa ushindi wa hivi karibuni wa chama cha an-Nahdha nchiniTunisia chini ya anwani ya 'kuenezwa Uislamu wa Kisiasa.' Limesema kwamba wananchi wa Tunisia walishiriki kwa wingi katika uchaguzi wa hivi karibuni ambapo asilimia 90 ya watu milioni 4.1 waliotimiza masharti ya kupiga kura walishiriki.
Gazeti hilo la Uingereza limesema kuwa uchaguzi huo ulifanyika kwa uwazi na uhuru mkubwa jambo ambalo halijawahi kushuhudiwa nchini humo tokea ijipatie uhuru kutoka kwa mkoloni Mfaransa.
Gazeti hilo limeendelea kuandika kwamba jambo hilo limezitia wasiwasi mkubwa nchi za Magharibi kwa kutilia maanani kwamba bunge la nchi hiyo litakalokuwa na wanachama 218 ndilo litakalokuwa na jukumu la kubuni katiba mpya ya nchi. Linasema, wasiwasi huo umeendelea kuongezeka kwa kutilia maanani kwamba Waislamu pia wanatazamiwa kushinda uchaguzi ujao wa Misri.
Nchi za Magharibi zimebainisha wasiwasi wao kuhusiana na kuongezeka kwa wimbi la mwamko wa Kiislamu katika nchi zilizokuwa zikitawaliwa na vibaraka wao na hasa ikizingatiwa kuwa viongozi wa wanamapinduzi nchini Libya wametangaza wazi kwamba wanataka kutawaliwa na sheria za Kiislamu. 887596